04/11/2009 8.42.16


Upendo wa Kristo unalibidisha Kanisa kuwajali na kuwasaidia wakimbizi na wahamiaji


|

Askofu mkuu Antonio Maria Vegliò, Rais wa Baraza la Kipapa la huduma za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji, wakimbizi na watu wasiokuwa na makazi amesema, Baraza lake limeandaa Kongamano la sita la kimataifa kwa ajili ya shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na wakimbizi, litakalofanyika mjini Vatican kuanzia tarehe 9 - 12 Novemba, 2009.
Kongamano hili linapania kutoa mwelekeo mpya wa kichungaji kwa ajili ya wakimbizi na wahamiaji katika ulimwengu wa utandawazi, miaka mitano tangu ilipochapishwa hati ya kichungaji; Erga Migrantes Caritas Christi: upendo wa Kristo unatuwajibisha kwa ajili ya wakimbizi, kutoka katika Baraza hilo.
Kanisa linapenda kuwa na mwelekeo mpana zaidi kuhusu tatizo la wahamiaji na wakimbizi duniani, kwa kuuangalia ustaarabu wa mtu, m aana ya maisha, uhuru na usalama, mahangaiko, ubaguzi wa kila aina pamoja na woga. Mambo haya anasema Askofu mkuu Vegliò yanaweza kutoweka katika ulimwengu wa utandawazi ikiwa kama haki msingi za binadamu zitalindwa na kuheshimiwa.
Utandawazi umeleta mafanikio makubwa katika nyanja mbali mbali za maisha, lakini pia kuna haja ya kuendelea kuboresha mwingiliano wa utamaduni, afya na hali ya maisha bila kusahahu kupambana na magonjwa yanayokwenda sambamba na madhara ya vita. Ni changamoto ya kuendelea kuboresha miundo mbinu, usalama na mwingiliano wa watu katika ulimwengu wa utandawazi unaosaidiwa zaidi na maendeleo ya sayansi na teknolojia katika nyanja za mawasiliano ya jamii.
Pamoja na mafanikio haya kuna haja bado ya kuendelea kutambua na kuthamini tunu msingi za maisha ya binadamu, uhuru, nafasi na dhamana ya wanawake, uvumilivu, mshikamano mambo yanayowaunganisha watu kwa pamoja, ili kupinga ubaguzi na tamaduni zote zinazokwenda kinyume cha ujenzi wa amani, utulivu na usawa katika jamii, ili kukuza na kudumisha demokrasia.
Askofu mkuu Vegliò anasema, Jumuiya ya Kimataifa na kitaifa imekuwa ikiyashughulikia masuala haya katika ngazi mbali mbali, ili kuboresha hali na maisha ya wakimbizi na wahamiaji mintarafu haki zao msingi. Katika miaka ya hivi karibuni mwanadamu amefaulu kufikia kiwango kikubwa cha maendeleo, lakini bado anakabiliana na changamoto za maisha ya upweke hasi, kielelezo cha watu kukata tamaa, kutoridhika na kusongwa mno na mawazo.
Bado hakuna utulivu wa haki jamii, ndoto ya watu wengi duniani. Watu wengi duniani wanaendelea anasema Askofu mkuu Vegliò, kukumbana na vita, magonjwa na njaa; kuchechemea kwa uchumi na mambo ambayo yanahatarisha afya na uhuru wa mtu.
Utandawazi umesaidia kuunda soko pana zaidi la ajira, hali inayowafanya watu wengi zaidi kuhama kutoka katika nchi zao wakitafuta maisha bora zaidi dhidi ya umaskini, majanga asilia, misigano ya kimataifa, bila kusahahu madhulumu ya kisiasa na kidini. Tatizo la wahamiaji linagusa undani wa uwajibikaji wa kimaadili na mwelekeo mpya wa hali ya uchumi kimataifa, kwa kuwa na ugawi mzuri zaidi wa rasilimali ya dunia. Kanisa linawajibika kulinda na kutetea utu na heshima ya mwanadamu, hasa zaidi wanyonge ndani ya jamii.
Askofu mkuu Antonio Maria Vegliò anasema kongamano la sita la kimataifa kwa ajili ya wahamiaji na wakimbizi linatafuta mmwelekeo mpya na mpana zaidi katika shughuli za kichungaji kwa wahamiaji na wakimbizi; kwa kuzingatia majadiliano ya kidini na kiekumene, heshima na utu wa kila mwanadamu, mshikamano na haki; amani na utulivu; haki sawa na majukumu sawa.
Mama Kanisa anaendelea katika h ali ya unyenyekevu kuangalia sababu zinazopelekea kuibuka kwa wimbi kubwa la wakimbizi na wahamiaji, ili kuwaonjesha huruma na upendo wake, hasa kwa wahanga wa biashara haramu ya binadamu, wahamiaji na wakimbizi wa kisiasa. Mama Kanisa anajisikia kuwa na wajibu wa kuwalinda na kuwatetea katika hali zao mbali mbali.
|