05/11/2009 8.39.08


Vijana: Ubinafsi ni sumu ya maendeleo!


|

Ubinafsi na mwono tenge katika maisha ya vijana ni sumu ya maendeleo ya vijana ndani ya jamii na katika harakati za ujenzi wa jamii inayosimikwa katika upatanisho, haki na amani.
Ni changamoto endelevu inayoendelea kutinduliwa na Padre Flavian Kassala Matindi, kutoka Chuo Kikuu cha Kipapa cha Wasalesiani mjini Roma, katika mfululizo wa makala zake kwa vijana, kama sehemu ya majiundo endelevu. Ninakusihi usikose kuwashirikisha wengine utamu wa mada hizi kwani, utamu wa "Sindimba" ni kucheza mwenyewe. Leo tunafunga mjadala wetu juu ya vijana kama tunu ya haki, amani na upatanisho katika Afrika na ulimwengu kwa ujumla. Baada ya kuwa tumeona thamani ya upekee, na nafasi yetu katika jamii leo tunaangalia sifa nyingine inayounganisha sifa hizi mbili na kuzipatia mwelekeo halisi katika maisha yetu ya kila siku. Si jingine bali ni uwezo wa kila kijana kuvuka mipaka ya maisha yaliyojengwa katika matumaini ya dunia hii tu na kufikia lengo hasa la Muumba aliyetupatia zawadi hizi mbili kuu.
Ujana hauwezi kulinganishwa na bango la matangazo ambapo kila mwenye haja yake anautumia kadri apendavyo. Wala si kipindi kitumikacho kana kwamba hakina mmiliki, hali ambayo inajidhihirisha katika jamii ambazo vijana wamekuwa wakitumika hasa katika mambo ya aibu na ya hatari kama vile vita, na biashara zote haramu. Na ndiyo maana kuna haja kubwa ya kuangalia na kuzichambua lugha kama vile, 'kila mtu anafanya hivi', 'vijana wote wanasema hivi', n.k.
Mwongozo wa maisha ya ujana, hasa katika kutafuta haki, amani na upatanisho wa kweli hauna budi kuwa na mwelekeo halisi. Ni mwongozo unaopatikana tu iwapo tutakuwa tayari kuingia ndani mwa nafsi zetu na kugundua sauti inayotuelekeza na kutufafanulia nini cha kufanya na nini cha kuacha. Ni sauti inayoweza kupotea pia iwapo hatutakuwa makini kuisikiliza na kutekeleza kile tunachokisikia na kukitendea kazi.
Wapendwa vijana, ni mwaliko wa kudumisha maisha ya tafakari na muungano na Mungu katika maisha yetu ya kidini. Hakuna namna nyingine tunayoweza kufikia kukamilisha haki na sifa yetu ya kuwa tunu katika jamii iwapo maisha yetu hayaongozwi na kweli za kidini. Amani, upendo, furaha na upatanisho wa kweli vinapatikana tu iwapo maisha yetu yatakuwa yanaongozwa na tunu hizi ambazo ni za kiinjili kweli.
Kwa asili binadamu ana hulka ya kutafuta kujilindia himaya yake hata kama ni kwa kulipiza kisasi. Lakini katika muungano wetu na Mungu, ambao ni zawadi tuipatayo katika maisha ya kidini pekee yake, tunaweza kusamehe kweli na kupatana katika tofauti zetu bila kuvunja tunu za haki na amani.
Na ukweli unabaki kuwa vijana katika nchi masikini kama za Afrika tumekwisha tumika vya kutosha katika mambo ambayo yanatupotezea hata tunu ndogo tulizonazo. Sasa ni kipindi cha kusema basi. Na hili tunaliweza tu iwapo maisha yetu yataongozwa na tunu za kiinjili. Hakuna haja ya kuendelea kuwa vyombo vya vita kwani sisi si silaha.
Katika ujumbe wake kwa adhimisho la 21 ya siku ya vijana duniani, Papa Benedikto 16 anaeleza wazi kuwa dunia ina haja ya kizazi kipya cha mitume waliojengeka katika kusikiliza neno la Mungu. Ni ujumbe unaotujia sisi sote hasa katika kipindi hiki tunapoungana na Kanisa zima la Afrika katika kutafuta haki, amani na upatanisho wa kweli.
Sisi ndio mitume halisi wa mwaliko huo, sisi ndio watekelezaji wa safari hii mpya kwa bara letu. Lakini ni wazi hatuwezi kuifanya peke yetu. Daima tuna haja ya kujenga na kutafuta kila siku nguvu na mwongozo wa kushinda vikwazo vipya katika Maandiko Matakatifu.
|