05/11/2009 9.12.28


Tatizo la wakimbizi na wahamiaji linapaswa kushughulikiwa kimataifa ili kupata ufumbuzi wa kudumu


|

Askofu mkuu Agostino Marchetto, Katibu mkuu wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum anasema, ili kukabiliana na wimbi la ongezeko la wahamiaji na wakimbizi, kuna haja kwa Jumuiya ya Kimataifa kujenga na kukuza kanuni ya auni.
Askofu mkuu Marchetto alikuwa anachangia mada kwenye kongamano kuhusu uhamiaji na maendeleo lililoanza mapema juma hili na kumalizika siku ya alhamisi mjini Athens, Ugriki. Jambo la msingi ni kuhakikisha kwamba, binadamu anatambuliwa na kuheshimiwa utu wake kabla hata ya kuanza kufikiri mambo mengine na kwamba ana haki zake msingi.
Haki na mafao ya wengi ni kanuni nyingine zinazobainishwa na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika kukabiliana na wimbi la ongezeko la wakimbizi na wahamiaji katika ulimwengu wa utandawazi. Anasema, kanuni ya mshikamano ikiheshimiwa na kuthaminiwa, bila shaka wahamiaji na wakimbizi wanaweza kupata nafuu katika maisha yao na hivyo kuchangia katika nchi wahisani pamoja na kusaidia juhudi za maendeleo ya nchi zao asilia.
Askofu mkuu Agostino Marchetto anakazia umuhimu wa kudumisha mwingiliano wa kitamaduni na kiuchumi ni changamoto ya kukoleza moyo na tabia ya ugunduzi inayokuwa pia ni chombo cha uhuru binafsi kama anavyoelezea Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika Barua yake ya kichungaji Ukweli katika upendo; "Caritas In Veritate".
Uhamiaji ni tatizo na changamoto kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa kwani hili ni tatizo linalovuka mipaka ya kitaifa na hivyo ufumbuzi wake unahitaji pia mwelekeo wa kimataifa, kwa kutambua kwamba, binadamu ni familia moja inayofanya kazi katika moyo wa umoja kutokana na asili yao.
|