05/11/2009 9.23.15


Mji wa Yerusalem hauna budi kuwa ni kitovu cha amani na suluhu ya migogoro katika Nchi Takatifu


|

Askofu mkuu Celestino Migliore, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa amesema, Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia wakimbizi wa Palestina, mwaka huu linaadhimisha miaka sitini tangu lilipoanzishwa, changamoto ya kukazia jitihada za kutafuta amani katika maeneo ya Palestina.
Askofu mkuu Migliore ameyasema hayo mapema wiki hii, alipokuwa anachangia mjadala katika kikao cha sitini na nne cha Baraza kuu la Umoja wa Mataifa kinachoendelea Jijini New York. Kinzani na machafuko ya kisiasa Nchi Takatifu ni kielelezo cha wazi kabisa cha pande mbili zinazohusika kutotaka kuzingatia majadiliano na hatimaye kutafuta ufumbuzi wa kudumu juu ya mgogoro wa watu wa Palestina, ili kudumisha haki na amani eneo la Mashariki ya Kati.
Askofu mkuu Migliore ameiasa Jumuiya ya Kimataifa kuzidisha juhudi za majadiliano ili kumaliza uhasama na chuki baina ya pande hizi mbili. Mji wa Yerusalemu kama kielelezo cha amani, lazima uwe ni sehemu ya suluhu ya matatizo huko Nchi Takatifu, miongoni mwa pande hizi mbili zinazoendelea kusigana. Amani ya kudumu inayopata chimbuko lake katika moyo wa mwanadamu kwa njia ya majadiliano na wala si kwa kulazimishana itaweza kuzaa matunda yanayokusudiwa.
|