07/11/2009 10.05.47


Kanisa laomba nafasi zaidi katika matumizi ya njia za mawasiliano ya jamii Cuba


|

Askofu mkuu Claudio Mario Celli, Rais wa Baraza la Kipapa la Mawasiliano ya Jamii, wakati wa ziara yake ya kichungaji nchini Cuba anaiomba Serikali ya Cuba kutoa nafasi kwa Kanisa ili kuweza kutumia kwa ukamilifu zaidi vyombo vya upashanaji habari ili liweze kutekeleza dhamana yake ya Uinjilishaji wa kina unaogusa mahitaji ya mtu mzima kiroho na kimwili.
Bado kuna vikwazo vingi katika matumizi ya vyombo vya mawasiliano ya jamii nchini Cuba. Ombi kama hili lilikkwisha wahi kutolewa pia na Kardinali Tarcisio Bertone, katibu mkuu wa Vatican alipotembelea Cuba, kunako mwaka 2008.
Askofu mkuu Celli anasema, kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya kisasa, Kanisa linapaswa kuendelea kutumia kwa ukamilifu fursa hii itakayoliwezesha kufikisha ujumbe wake kwa hadhira inayokusudiwa kwa muda mfupi. Ni changamoto hata kwa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki kuhakikisha kwamba, yanatumia maendeleo ya sayansi na Teknolojia kikamilifu.
Kuna kizazi cha watu wasiopenda kusoma, hawa wanaweza kupata ujumbe wa Kanisa kwa njia ya Televisheni au Radio. Lakini kuna watu wanaopenda kujichimbia katika maarifa hawa wanaweza kufikiwa kwa njia ya mtandao. Askofu mkuu Celli anaendelea kulihimiza Kanisa kutumia fursa hii kikamilifu hasa katika utamaduni wa mtandao kwa kuwa na lugha inayokwenda sambamba na maendeleo haya yanayowaunganisha watu kutoka kila kabila, lugha na jamaa.
Kanisa anasema Askofu mkuu Claudio Maria Celli litaendelea kufanya majadiliano ya kina na Serikali ya Cuba ili kupata mwanya zaidi katika matumizi ya vyombo vya mawasiliano ya kijamii.
Majadiliano haya, hayana budi kwenda sambamba na majiundo ya matumizi bora ya mawasiliano pamoja na kuachana na ule mtindo wa kufanya kazi kwa kificho, bali sasa wajitahidi kushirikiana na mashirika mengine ili kuweza kufika mbali zaidi, kwa kutumia vyema rasilimali iliyopo ndani ya Kanisa. Waandaliwe makleri na walei watakaoifanya kazi hii kwa uaminifu mkubwa, ili kufikisha mahudhui ya Kanisa kwa hadhira inayokusudiwa.
Akizungumza na waandhishi wa habari siku ya ijumaa tarehe 6 Novemba, 2009, Askofu mkuu Celli ameridhishwa na mapokezi aliyopata kutoka kwa viongozi wa Kanisa na Serikali kwa ujumla, hali inayotia matumaini kwamba, vikwazo vilivyojitokeza katika historia ya Kanisa nchini Cuba kuhusu matumizi ya vyombo vya mawasiliano ya kijamii vitaweza kupatiwa ufumbuzi wa haraka. Katika ziara hii, Askofu mkuu Celli aliambatana na Askofu mkuu Giovanni Angelo Becciu, Balozi mpya wa Vatican nchini Cuba.
|